YouVersion Logo
Search Icon

Zaburi 10

10
Sala dhidi ya udhalimu
1Ee Mwenyezi-Mungu, mbona wasimama mbali?
Kwa nini wajificha wakati tumo taabuni?
2Kwa kiburi waovu wanawatesa maskini;
njama zao ziwanase wao wenyewe.
3Mwovu hujisifia tamaa zake mbaya,
mtu wa tamaa hulaani na kumkataa Mwenyezi-Mungu.
4Katika majivuno yake husema: “Mungu hatagundua.”
Mawazo yake yote ni: “Hakuna Mungu.”
5Njia za mwovu hufanikiwa daima;
kwake hukumu zako ziko mbali na mawazo yake,
na huwadharau maadui zake wote.
6Huwaza moyoni: “Sitakuwa na wasiwasi;
sitapatwa na dhiki maishani.”
7 # Taz Rom 3:14 Kinywa chake kimejaa laana, udanganyifu na dhuluma;
mwepesi kusema maneno ya kuchukiza na maovu.
8Hujificha vijijini huku anaotea,
amuue kwa siri mtu asiye na hatia.
Yuko macho kumvizia mnyonge;
9huotea mafichoni mwake kama simba.
Huvizia apate kuwakamata maskini;
huwanasa kwa mtego wake na kuwachukua.
10Mnyonge huvamiwa na kuangushwa chini;
huangushwa kwa ukatili wa mtu mwovu.
11Mwovu huwaza moyoni mwake: “Mungu amesahau;
ameficha uso wake, haoni kitu!”
12Inuka, ee Mwenyezi-Mungu, uwaadhibu;
usiwasahau wanaodhulumiwa.
13Ee Mungu, kwa nini mwovu anakudharau,
na kusema ati hutamfanya awajibike?
14Lakini wewe wawaona wenye dhiki na shida;
nawe daima uko tayari kuwasaidia.
Mnyonge anakutegemea wewe, ee Mungu,
wewe umekuwa daima msaada wa yatima.
15Uzivunje nguvu za mtu mwovu;
ukomeshe uovu wake wote, usiwepo tena.
16Mwenyezi-Mungu ni mfalme milele na milele!
Mataifa yasiyomjua yatatoweka nchini mwake.
17Ee Mwenyezi-Mungu, wapokea dua za mnyonge;
wampa moyo na kumtegea sikio.
18Utawatendea haki yatima na wanaodhulumiwa,
binadamu aliye udongo asiweze tena kuleta hofu.

Currently Selected:

Zaburi 10: BHN

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in