Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Matendo 15

15
Baraza la Yerusalemu na matokeo yake
(Matendo 15:1-35)
Baraza la Yerusalemu
1Baadhi ya watu wakashuka Antiokia kutoka Yudea, nao wakawa wanawafundisha waumini: “Msipotahiriwa kulingana na desturi aliyofundisha Musa, hamwezi kuokoka.” 2Baada ya Paulo na Barnaba kutokubaliana nao kukawa na mabishano makali, Paulo na Barnaba na baadhi ya wengine miongoni mwao wakachaguliwa kwenda Yerusalemu ili kujadiliana jambo hili na mitume na wazee. 3Hivyo wakatumwa na waumini. Wakapitia Foinike na Samaria, wakielezea jinsi watu wa Mataifa walivyoongoka. Habari hizi zikaleta furaha kubwa kwa ndugu wote. 4Walipofika Yerusalemu, walipokelewa na kundi la waumini na mitume pamoja na wazee. Ndipo Paulo na Barnaba wakawaarifu kila kitu Mungu alichokuwa amefanya kupitia kwao.
5Ndipo baadhi ya waumini waliokuwa wa dhehebu la Mafarisayo#15:5 Kundi la kidini la Wayahudi; walifuata Torati kwa dhati, hasa maagizo kuhusu utakaso. Pia waliamini katika malaika, ufufuo wa wafu, na kuja kwa Masihi ambaye atarejesha ufalme wa Daudi na ukuu wa taifa la Israeli. wakasimama na kusema, “Hao watu wa Mataifa lazima watahiriwe na waagizwe kutii Torati ya Musa.”
6Mitume na wazee wakakutana pamoja ili kufikiri jambo hili. 7Baada ya majadiliano mengi, Petro akasimama na kusema, “Ndugu zangu, mnajua kwamba siku za kwanza Mungu alinichagua ili kwa midomo yangu watu wa Mataifa wapate kusikia ujumbe wa Injili na kuamini. 8Mungu, ajuaye mioyo ya watu, alionesha kwamba anawakubali kwa kuwapa Roho Mtakatifu wa Mungu kama vile alivyotupatia sisi. 9Mungu hakutofautisha kati yetu na wao, bali alitakasa mioyo yao kwa imani. 10Sasa basi, mbona mnataka kumjaribu Mungu kwa kuweka nira shingoni mwa wanafunzi ambayo baba zetu wala sisi hatukuweza kuibeba? 11Lakini sisi tunaamini ya kuwa tunaokolewa kwa neema ya Bwana wetu Isa Al-Masihi, kama wao wanavyookolewa.”
12Kusanyiko lote wakakaa kimya, wakawasikiliza Paulo na Barnaba wakieleza jinsi Mungu alivyowatumia kutenda ishara na maajabu kwa watu wa Mataifa. 13Walipomaliza kunena, Yakobo akasema, “Ndugu zangu, nisikilizeni. 14Simoni amekwisha kutueleza jinsi Mungu, kwa mara ya kwanza alivyoonesha kuhusika kwa kujichagulia watu kutoka watu wa Mataifa kwa ajili ya Jina lake. 15Maneno ya manabii yanakubaliana na jambo hili, kama ilivyoandikwa:
16“ ‘Baada ya mambo haya nitarudi,
nami nitajenga upya
nyumba ya Daudi iliyoanguka.
Nitajenga tena magofu yake
na kuisimamisha,
17ili wanadamu wengine wote
wapate kumtafuta Mwenyezi Mungu,
hata wale watu wa Mataifa wote
ambao wanaitwa kwa Jina langu,
asema Mwenyezi Mungu, anayefanya mambo haya,’#15:17 Amosi 9:11, 12
18ambayo yamejulikana tangu zamani.
19“Kwa hivyo uamuzi wangu ni kwamba, tusiwataabishe watu wa Mataifa wanaomgeukia Mungu. 20Badala yake, tuwaandikie kwamba wajiepushe na vyakula vilivyonajisiwa kwa kutolewa sanamu, wajiepushe na uasherati, au kula mnyama aliyenyongwa, na damu. 21Kwa maana katika kila mji kwa vizazi vilivyopita, Musa amekuwa na wale wanaotangaza sheria yake kwa kuwa imekuwa ikisomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi#15:21 Nyumba za ibada na mafunzo. kila Sabato.”
Barua kwa waumini wa Mataifa
22Mitume na wazee, pamoja na kundi la waumini wote, wakaamua kuwachagua baadhi ya watu wao na kuwatuma Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba. Wakamchagua Yuda aitwaye Barsaba, pamoja na Sila, watu wawili waliokuwa viongozi miongoni mwa ndugu. 23Wakatumwa na barua ifuatayo:
Sisi mitume na wazee, ndugu zenu.
Kwa waumini wa Mataifa mlio Antiokia, Siria na Kilikia.
Salamu.
24Tumesikia kwamba kuna baadhi ya watu waliokuja huko kutoka kwetu bila ruhusa yetu na kuwasumbua, wakiyataabisha mawazo yenu. 25Hivyo tumekubaliana wote kuwachagua baadhi ya watu na kuwatuma kwenu pamoja na wapendwa wetu Barnaba na Paulo, 26watu ambao wamehatarisha maisha yao kwa ajili ya jina la Bwana wetu Isa Al-Masihi. 27Kwa hiyo tunawatuma Yuda na Sila, kuthibitisha kwa maneno ya mdomo mambo haya tunayowaandikia. 28Kwa maana imempendeza Roho wa Mungu na sisi tusiwatwike mzigo wowote mkubwa zaidi ya mambo haya yafuatayo ambayo ni ya lazima: 29Kwamba mjiepushe na vyakula vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, au kula nyama ya mnyama aliyenyongwa, na mjiepushe na uasherati. Mkiyaepuka mambo haya, mtakuwa mmefanya vyema.
Kwaherini.
30Hivyo wakaagwa, wakashuka kwenda Antiokia. Baada ya kulikusanya kundi la waumini pamoja, wakawapa ile barua. 31Baada ya hao watu kuisoma, wakafurahishwa sana kwa ujumbe wake wa kutia moyo. 32Yuda na Sila, ambao wenyewe walikuwa manabii, wakanena maneno mengi ya kuwatia moyo na kuwajenga waumini katika imani. 33Baada ya kukaa huko Antiokia kwa muda, wakaagwa kwa amani na wale ndugu ili waende kwa wale waliowatuma. [ 34Lakini Sila bado akaendelea kukaa huko.]#15:34 Maandiko mengine ya kale hayana maneno haya. 35Lakini Paulo na Barnaba walibaki Antiokia ambako wao pamoja na wengine wengi walifundisha na kuhubiri neno la Bwana Isa.
Safari ya pili ya Paulo kueneza Injili
(Matendo 15:36–18:22)
Paulo na Barnaba wagawanyika
36Baada ya muda, Paulo akamwambia Barnaba, “Turudi tukawatembelee ndugu katika miji yote tuliyohubiri neno la Bwana Isa tuone jinsi wanavyoendelea.” 37Barnaba alitaka wamchukue Yohana aitwaye Marko waende naye. 38Lakini Paulo aliona si vyema kwa sababu aliwahi kuwaacha walipokuwa huko Pamfilia, hakutaka kuendelea kufanya kazi naye. 39Pakatokea ubishi mkali kati ya Paulo na Barnaba kuhusu jambo hili, hivyo wakagawanyika. Barnaba akamchukua Yohana Marko wakasafiri baharini kwenda Kipro. 40Lakini Paulo akamchagua Sila na akaondoka baada ya ndugu kuwatakia neema ya Bwana Isa. 41Akapitia Siria na Kilikia, akiimarisha makundi ya waumini ya huko.

Iliyochaguliwa sasa

Matendo 15: NENO

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia