Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Wafalme 7:1-14

1 Wafalme 7:1-14 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)

Naye Sulemani alikuwa katika kuijenga nyumba yake mwenyewe miaka kumi na mitatu, akaimaliza nyumba yake yote. Kwa kuwa aliijenga nyumba ya mwitu wa Lebanoni; mikono mia urefu wake, na mikono hamsini upana wake, na mikono thelathini kwenda juu kwake, juu ya safu nne za nguzo za mwerezi, na mihimili ya mwerezi juu ya nguzo. Ikafunikwa juu kwa mwerezi juu ya mihimili arobaini na mitano, iliyokuwa juu ya nguzo; kumi na mitano kwa safu. Na madirisha yalikuwako safu tatu, mwangaza kuelekea mwangaza katika madaraja matatu. Na milango yote na miimo ilikuwa ya mraba, ilivyoangaziwa; na mwangaza kuelekea mwangaza katika madaraja matatu. Akaifanya baraza ya nguzo; mikono hamsini urefu wake, na mikono thelathini upana wake; na ukumbi mbele yake; na nguzo na mihimili minene mbele yake. Akaifanya baraza ya kiti cha enzi, ili ahukumu ndani yake, ndiyo baraza ya hukumu; nayo ikafunikwa mwerezi tangu sakafu mpaka dari. Nayo nyumba yake atakayokalia, katika behewa nyingine iliyokuwa ndani kupita baraza, ilikuwa ya kazi kama hiyo. Tena akamjengea nyumba binti Farao, (ambaye Sulemani alikuwa amemwoa), mfano wa ile baraza. Hizi zote zilikuwa za mawe ya thamani, mawe ya kuchongwa, sawasawa na cheo, yaliyokatwa kwa misumeno, ndani na nje, tangu msingi hata mawe ya juu, na nje vile vile hata behewa kuu. Nao msingi ulikuwa wa mawe ya thamani, mawe makubwa, mawe mikono kumi, na mawe ya mikono minane. Na juu kulikuwa na mawe ya thamani, mawe ya kuchongwa, sawasawa na cheo, na mierezi. Na behewa kubwa pande zote ilikuwa na safu tatu za mawe ya kuchongwa, na safu moja ya mihimili ya mierezi; mfano wa behewa ya ndani ya nyumba ya BWANA, na ukumbi wa nyumba. Mfalme Sulemani akatuma watu kumleta Huramu kutoka Tiro. Naye alikuwa mwana wa mwanamke mjane wa kabila ya Naftali, na babaye alikuwa mtu wa Tiro, mfua shaba; naye alikuwa mwingi wa hekima na akili, mstadi wa kufanya kazi zote za shaba. Akamfikilia mfalme Sulemani, akamfanyia kazi yake yote.

1 Wafalme 7:1-14 Neno: Bibilia Takatifu (NEN)

Ilimchukua Solomoni miaka kumi na mitatu kukamilisha ujenzi wa Jumba lake la kifalme. Alijenga Jumba la Kifalme la Msitu wa Lebanoni, urefu wake ulikuwa dhiraa 100, upana wake dhiraa hamsini na kimo chake dhiraa thelathini, likiwa na safu nne za nguzo za mierezi zikishikilia boriti za mierezi zilizorembwa. Ilipauliwa kwa mierezi juu ya boriti zile zilizolala juu ya nguzo arobaini na tano, kumi na tano kwa kila safu. Madirisha yake yaliwekwa juu kwa safu tatu, yakielekeana. Milango yote ilikuwa na miimo ya mstatili, ilikuwa upande wa mbele katika safu tatu, ikielekeana. Akajenga ukumbi wa nguzo, ambao urefu wake ulikuwa dhiraa hamsini na upana wake dhiraa thelathini. Mbele ya jengo hilo kulikuwepo baraza. Mbele ya baraza kulikuwepo na nguzo na paa lililoningʼinia. Akajenga ukumbi wa kiti cha enzi, Ukumbi wa Hukumu, mahali ambapo angelitolea hukumu, akaufunika kwa mierezi kutoka sakafuni hadi darini. Kwenye jumba la kifalme ambamo angeliishi, aliiweka nyuma zaidi, ikiwa na mjengo wa aina moja na hiyo nyingine. Pia Solomoni akajenga jumba la kifalme linalofanana na huo ukumbi mkubwa kwa ajili ya binti Farao, aliyekuwa amemwoa. Ujenzi huu wote, kuanzia nje mpaka kwenye ua mkuu na kuanzia kwenye msingi hadi upenuni, ulifanywa kwa mawe ya ubora wa hali ya juu yaliyokuwa yamechongwa kwa vipimo na kusawazishwa kwa msumeno nyuso zake za ndani na za nje. Misingi iliwekwa kwa mawe makubwa yaliyo bora, yenye urefu wa dhiraa kumi na mengine yenye urefu wa dhiraa nane Sehemu za juu kulikuwepo na mawe yenye ubora wa hali ya juu, yaliyokatwa kwa vipimo na boriti za mierezi. Ule ua mkuu ulizungukwa na ukuta wa safu tatu za mawe yaliyochongwa na safu moja ya boriti za mierezi zilizorembwa, kama ulivyokuwa ua wa ndani wa Hekalu la BWANA na baraza yake. Mfalme Solomoni akatuma watu Tiro kumleta Hiramu, ambaye mama yake alikuwa mjane kutoka kabila la Naftali na baba yake alikuwa mtu wa Tiro tena fundi wa shaba. Hiramu alikuwa na ustadi wa hali ya juu na mzoefu katika aina zote za kazi ya shaba. Alikuja kwa Mfalme Solomoni na kufanya kazi zake zote alizopangiwa.

1 Wafalme 7:1-14 Biblia Habari Njema (BHN)

Solomoni alijijengea ikulu, nayo ilimchukua miaka kumi na mitatu kumalizika. Kisha, akajenga jengo lililoitwa Nyumba ya Msitu wa Lebanoni. Urefu wake ulikuwa mita 44.5, upana wake mita 22.25, na kimo chake mita 13.5. Ilikuwa imejengwa juu ya safu 3 za nguzo za mierezi, nguzo ambazo zilishikilia boriti za mierezi kwa upande wa juu. Kila safu ilikuwa na nguzo 15; basi zote pamoja zilikuwa nguzo 45. Vyumba vilivyojengwa juu ya nguzo hizo, alivitilia dari ya mbao za mierezi. Kulikuwa na safu tatu za madirisha yaliyoelekeana. Milango yote ilikuwa ya mraba, na miimo ya madirisha hayo yaliyoelekeana ilikuwa pia ya mraba. Alijenga ukumbi wa nguzo, ambao urefu wake ulikuwa mita 22.25, na upana wake mita 13.5. Kwenye sehemu ya mbele ya jengo hilo kulikuwa na sebule. Mbele ya sebule kulikuwa na nguzo; na mbele ya nguzo kulitokeza paa dogo. Solomoni alijenga ukumbi wa kiti cha enzi ambamo aliamulia kesi za watu. Huu uliitwa pia Ukumbi wa Hukumu. Ulikuwa umepambwa kwa mbao za mierezi kutoka sakafu mpaka dari. Nyumba yake ya kukaa mwenyewe, iliyokuwa nyuma ya Ukumbi wa Hukumu, ilikuwa imejengwa kama zile nyingine. Solomoni pia alijenga nyumba kama ukumbi huo kwa ajili ya binti Farao, ambaye alikuwa amemwoa. Majengo hayo yote yalijengwa kwa mawe ya thamani kutoka msingi mpaka juu, mawe ambayo yalikuwa yamechongwa kwa vipimo maalumu, na kukatwa kwa msumeno upande wa ndani na wa nje. Msingi ulikuwa wa mawe ya thamani na makubwa yenye urefu wa mita 3.5, na upana mita 4.5. Sehemu za juu zilijengwa kwa mawe mengine yaliyochongwa kwa vipimo maalumu, na kwa mbao za mierezi. Ua wa nyumba ya mfalme ulikuwa na kuta zenye safu moja ya mbao za mierezi na safu tatu za mawe ya kuchongwa kila moja; ndivyo ilivyokuwa hata kwa ua wa ndani wa nyumba ya Mwenyezi-Mungu na kwa ukumbi wa nyumba. Kisha mfalme Solomoni alimwita Hiramu kutoka Tiro. Huyo, alikuwa mwana wa mjane wa kabila la Naftali, na baba yake alikuwa mkazi wa Tiro, mfua shaba. Hiramu alikuwa na hekima nyingi na akili, na fundi stadi wa kazi yoyote ya shaba. Basi, alikuja kwa mfalme Solomoni, akamfanyia kazi yake yote.

1 Wafalme 7:1-14 Swahili Revised Union Version (SRUV)

Naye Sulemani alikuwa katika kuijenga nyumba yake mwenyewe miaka kumi na mitatu, akaimaliza nyumba yake yote. Kisha alijenga nyumba ya msitu wa Lebanoni; mikono mia moja urefu wake, na mikono hamsini upana wake, na mikono thelathini kwenda juu kwake, juu ya safu nne za nguzo za mwerezi, na mihimili ya mwerezi juu ya nguzo. Ikafunikwa juu kwa mwerezi juu ya mihimili arubaini na mitano, iliyokuwa juu ya nguzo; kumi na mitano kwa safu. Na madirisha yalikuwako safu tatu, mwangaza kuelekea mwangaza katika madaraja matatu. Na milango yote na miimo ilikuwa ya mraba, ilivyoangaziwa; na mwangaza kuelekea mwangaza katika madaraja matatu. Akaifanya baraza ya nguzo; mikono hamsini urefu wake, na mikono thelathini upana wake; na ukumbi mbele yake; na nguzo na mihimili minene mbele yake. Akaifanya baraza ya kiti cha enzi, ili ahukumu ndani yake, ndiyo baraza ya hukumu; nayo ikafunikwa mwerezi tangu sakafu mpaka dari. Nayo nyumba yake atakayokalia, katika behewa nyingine iliyokuwa ndani kupita baraza, ilikuwa ya kazi kama hiyo. Tena akamjengea nyumba binti Farao, (ambaye Sulemani alikuwa amemwoa), mfano wa ile baraza. Hizi zote zilikuwa za mawe ya thamani, mawe ya kuchongwa, sawasawa na cheo, yaliyokatwa kwa misumeno, ndani na nje, tangu msingi hata mawe ya juu, na nje vile vile hata behewa kuu. Nao msingi ulikuwa wa mawe ya thamani, mawe makubwa, mawe mikono kumi, na mawe ya mikono minane. Na juu kulikuwa na mawe ya thamani, mawe ya kuchongwa, kulingana na cheo, na mierezi. Na behewa kubwa pande zote ilikuwa na safu tatu za mawe ya kuchongwa, na safu moja ya mihimili ya mierezi; mfano wa behewa ya ndani ya nyumba ya BWANA, na ukumbi wa nyumba. Mfalme Sulemani akatuma watu kumleta Hiramu kutoka Tiro. Naye alikuwa mwana wa mwanamke mjane wa kabila la Naftali, na babaye alikuwa mtu wa Tiro, mfua shaba; naye alikuwa mwingi wa hekima na akili, stadi wa kufanya kazi zote za shaba. Akamfikia mfalme Sulemani, akamfanyia kazi yake yote.