Matendo 28:1-10
Matendo 28:1-10 Biblia Habari Njema (BHN)
Tulipokwisha fika salama kwenye nchi kavu, tuligundua kwamba kile kisiwa kinaitwa Malta. Wenyeji wa hapo walikuwa wema sana kwetu. Mvua ilikuwa inaanza kunyesha na kulikuwa na baridi, hivyo waliwasha moto, wakatukaribisha. Paulo aliokota mzigo mdogo wa kuni akawa anazitia motoni. Hapo, kwa sababu ya lile joto la moto, nyoka akatoka katika kuni akamnasa Paulo mkononi na kujishikilia hapo. Wenyeji wa pale walipokiona kile kiumbe kinaninginia kwenye mkono wake waliambiana, “Bila shaka mtu huyu amekwisha ua mtu, na ingawa ameokoka kuangamia baharini, ‘Haki’ haitamwacha aendelee kuishi!” Lakini Paulo alikikungutia kile kiumbe motoni na hakuumizwa hata kidogo. Wale watu walikuwa wakitazamia kwamba angevimba au angeanguka chini na kufa ghafla. Baada ya kungojea kwa muda mrefu bila kuona kwamba Paulo amepatwa na jambo lolote lisilo la kawaida, walibadilisha fikira zao juu yake, wakasema kuwa yeye ni mungu. Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya Publio, mkuu wa kile kisiwa. Publio alitukaribisha kirafiki, tukawa wageni wake kwa siku tatu. Basi, ikawa kwamba baba yake Publio alikuwa amelala kitandani, mgonjwa wa homa na kuhara. Paulo alikwenda kumwona na baada ya kusali, akaweka mikono yake juu ya mgonjwa, akamponya. Kutokana na tukio hilo, wagonjwa wote katika kile kisiwa walikuja wakaponywa. Watu walitupatia zawadi mbalimbali na wakati tulipoanza tena safari, walitia ndani ya meli masurufu tuliyohitaji.
Matendo 28:1-10 Swahili Revised Union Version (SRUV)
Tulipokwisha kuokoka, ndipo tulipojua ya kuwa kisiwa kile chaitwa Melita. Wenyeji wakatufanyia fadhili zisizokuwa za kawaida. Kwa maana waliwasha moto, wakatukaribisha sote, kwa sababu ya mvua iliyonyesha na kwa sababu ya baridi. Paulo alipokuwa amekusanya mzigo wa kuni, na kuuweka motoni, nyoka akatoka kwa ajili ya ule moto akamzongazonga mkononi. Wenyeji walipomwona yule nyoka akilewalewa mkononi, wakaambiana, Hakosi mtu huyu ni mwuaji; ambaye ijapokuwa ameokoka katika bahari haki haimwachi kuishi. Lakini yeye akamtukusia motoni asipate madhara. Wao wakadhani ya kuwa atavimba au kuanguka chini kwa kufa ghafla; na wakiisha kumwangalia sana, na kuona kwamba halimpati dhara lolote, wakageuka, wakasema kwamba yeye ni mungu. Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa, jina lake Publio; mtu huyu akatukaribisha kwa moyo wa urafiki, akatufanya wageni wake kwa muda wa siku tatu. Ikawa babake Publio alikuwa akiugua homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumponya. Yalipokwisha kutendeka hayo wengine waliokuwa na magonjwa katika kisiwa wakaja wakaponywa; nao wakatuheshimu kwa heshima nyingi; basi tulipoabiri wakatupakilia vitu vile tulivyokuwa na haja navyo.
Matendo 28:1-10 Maandiko Matakatifu ya Mungu Yaitwayo Biblia (SUV)
Tulipokwisha kuokoka, ndipo tulipojua ya kuwa kisiwa kile chaitwa Melita. Wenyeji wakatufanyia fadhili zisizokuwa za kawaida. Kwa maana waliwasha moto, wakatukaribisha sote, kwa sababu ya mvua iliyonyesha na kwa sababu ya baridi. Paulo alipokuwa amekusanya mzigo wa kuni, na kuuweka motoni, nyoka akatoka kwa ajili ya ule moto akamzonga-zonga mkononi. Wenyeji walipomwona yule nyoka akilewa-lewa mkononi, wakaambiana, Hakosi mtu huyu ni mwuaji; ambaye ijapokuwa ameokoka katika bahari haki haimwachi kuishi. Lakini yeye akamtukusia motoni asipate madhara. Wao wakadhani ya kuwa atavimba au kuanguka chini kwa kufa ghafula; na wakiisha kumwangalia sana, na kuona kwamba halimpati dhara lo lote, wakageuka, wakasema kwamba yeye ni mungu. Karibu na mahali pale palikuwa na mashamba ya mkuu wa kisiwa, jina lake Publio; mtu huyu akatukaribisha kwa moyo wa urafiki, akatufanya wageni wake kwa muda wa siku tatu. Ikawa babaake Publio alikuwa hawezi homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumpoza. Yalipokwisha kutendeka hayo wengine waliokuwa na magonjwa katika kisiwa wakaja wakapozwa; nao wakatuheshimu kwa heshima nyingi; basi tulipoabiri wakatupakilia vitu vile tulivyokuwa na haja navyo.
Matendo 28:1-10 Neno: Maandiko Matakatifu 2024 (NENO)
Baada ya kufika nchi kavu salama, ndipo tukafahamu kwamba jina la kile kisiwa ni Malta. Wenyeji wa kile kisiwa walituonesha ukarimu usio wa kawaida. Waliwasha moto na kutukaribisha sisi sote kwa sababu mvua ilikuwa inanyesha na kulikuwa na baridi. Paulo alikusanya mzigo wa kuni, na alipokuwa anaweka kuni kwenye moto, nyoka mwenye sumu akatoka humo kwa ajili ya joto na kujisokotea mkononi mwake. Wale wenyeji wa kile kisiwa walipomwona yule nyoka akining’inia mkononi mwa Paulo, wakaambiana, “Huyu mtu lazima awe ni muuaji, ingawa ameokoka kutoka baharini, haki haijamwacha aishi.” Lakini Paulo akamkung’utia yule nyoka ndani ya moto wala yeye hakupata madhara yoyote. Watu walikuwa wanangoja avimbe au aanguke ghafula na kufa. Lakini baada ya kungoja kwa muda mrefu na kuona kwamba hakuna chochote kisicho cha kawaida kilichomtokea, wakabadili mawazo yao na kuanza kusema kwamba yeye ni mungu. Basi karibu na sehemu ile, palikuwa na shamba kubwa la kiongozi mkuu wa kile kisiwa, aliyeitwa Publio. Alitupokea kwake, na akatuhudumia kwa ukarimu mkubwa kwa muda wa siku tatu. Baba yake Publio alikuwa mgonjwa kitandani, akiwa anaugua homa na kuhara damu. Paulo akaingia ndani ili kumwona na baada ya maombi, akaweka mikono juu yake na kumponya. Jambo hili lilipotukia, watu wote wa kisiwa kile waliokuwa wagonjwa wakaja, nao wakaponywa. Wakatupatia heshima nyingi, nasi tulipokuwa tayari kusafiri kwa meli, wakatupakilia vitu vyote tulivyokuwa tunavihitaji.