Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

1 Wafalme 8:1-11

1 Wafalme 8:1-11 NEN

Kisha Mfalme Solomoni akawaita mbele zake huko Yerusalemu wazee wa Israeli, viongozi wote wa makabila na wakuu wa jamaa za Waisraeli, ili walilete Sanduku la Agano la BWANA kutoka Sayuni, Mji wa Daudi. Wanaume wote wa Israeli wakakusanyika kwa Mfalme Solomoni wakati wa sikukuu ya mwezi wa Ethanimu, ndio mwezi wa saba. Wazee wote wa Israeli walipofika, makuhani wakajitwika Sanduku la Agano, nao wakalipandisha Sanduku la BWANA, na Hema la Kukutania pamoja na vyombo vyote vitakatifu vilivyokuwa ndani yake. Makuhani na Walawi wakavibeba, naye Mfalme Solomoni na kusanyiko lote la Israeli waliokusanyika kumzunguka walikuwa mbele ya hilo Sanduku, nao wakatoa dhabihu nyingi za kondoo na ngʼombe ambao idadi yao haikuwezekana kuandikwa au kuhesabiwa. Makuhani wakalileta Sanduku la Agano la BWANA hadi mahali pake ndani ya sehemu takatifu ndani ya Hekalu, yaani Patakatifu pa Patakatifu, na kuliweka chini ya mabawa ya makerubi. Makerubi yalitandaza mabawa yao juu ya mahali pa Sanduku la Agano na kutia kivuli Sanduku pamoja na mipiko yake ya kubebea. Mipiko hiyo ilikuwa mirefu sana kiasi kwamba ncha zake zilionekana kutoka Mahali Patakatifu mbele ya Patakatifu pa Patakatifu, lakini sio nje ya Mahali Patakatifu. Hiyo mipiko ipo hata leo. Ndani ya Sanduku hapakuwepo kitu kingine chochote isipokuwa zile mbao mbili za mawe ambazo Mose alikuwa ameziweka ndani yake huko Horebu, mahali ambapo BWANA alifanya Agano na Waisraeli baada ya kutoka Misri. Makuhani walipoondoka katika Mahali Patakatifu, wingu likajaza Hekalu la BWANA. Nao makuhani hawakuweza kufanya huduma yao kwa sababu ya lile wingu, kwa kuwa utukufu wa BWANA ulijaza Hekalu lake.

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na 1 Wafalme 8:1-11