Ezekieli 19
19
Maombolezo kwa ajili ya wakuu wa Israeli
1“Wewe fanya maombolezo kuhusu wakuu wa Israeli 2na useme:
“ ‘Tazama jinsi gani mama yako alivyokuwa simba jike
miongoni mwa simba!
Alilala katikati ya wana simba
na kulisha watoto wake.
3Alimlea mmoja wa watoto wake,
naye akawa simba mwenye nguvu.
Akajifunza kurarua mawindo
naye akala watu.
4Mataifa wakasikia habari zake,
naye akanaswa katika shimo lao.
Wakamwongoza kwa ndoana
hadi nchi ya Misri.
5“ ‘Mama yake alipongoja na kuona tumaini lake halitimiziki,
nayo matarajio yake yametoweka,
akamchukua mwanawe mwingine
na kumfanya simba mwenye nguvu.
6Alizungukazunguka miongoni mwa simba,
kwa kuwa sasa alikuwa simba mwenye nguvu.
Akajifunza kurarua mawindo
naye akala watu.
7Akabomoa ngome zao
na kuiharibu miji yao.
Nchi na wote waliokuwa ndani yake
wakatiwa hofu kwa kunguruma kwake.
8Kisha mataifa wakaja dhidi yake
kutoka sehemu zilizomzunguka.
Wakatanda nyavu zao kwa ajili yake,
naye akanaswa katika shimo lao.
9Wakamvutia kwenye tundu kwa kutumia ndoana,
wakamleta kwa mfalme wa Babeli.
Wakamfunga gerezani, hivyo kunguruma kwake
hakukusikika tena
katika milima ya Israeli.
10“ ‘Mama yako alikuwa kama mzabibu
katika shamba lako la mizabibu
uliopandwa kando ya maji,
ukiwa unazaa sana na wenye matawi mengi
kwa sababu ya wingi wa maji.
11Matawi yake yalikuwa na nguvu,
yaliyofaa kuwa fimbo ya mtawala.
Ulikuwa mrefu kupita miti mingine
katikati ya matawi manene;
ulionekana kwa urahisi
kwa ajili ya urefu wake
na wingi wa matawi yake.
12Lakini uling’olewa kwa hasira kali
na kutupwa chini.
Upepo wa mashariki uliufanya usinyae,
matunda yake yakapukutika,
matawi yake yenye nguvu yakanyauka
na moto ukayateketeza.
13Sasa umepandwa jangwani
katika nchi kame na ya kiu.
14Moto ulienea kuanzia mojawapo ya matawi yake makubwa
na kuteketeza matunda yake.
Hakuna tawi lenye nguvu lililobaki juu yake
linalofaa kuwa fimbo ya mtawala.’
Hili ndilo ombolezo, na litumike kama ombolezo.”
Iliyochaguliwa sasa
Ezekieli 19: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
![None](/_next/image?url=https%3A%2F%2Fimageproxy.youversionapistaging.com%2F58%2Fhttps%3A%2F%2Fweb-assets.youversion.com%2Fapp-icons%2Fsw.png&w=128&q=75)
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.