Yohana 11:1-45
Yohana 11:1-45 NENO
Basi mtu mmoja, jina lake Lazaro, alikuwa mgonjwa. Yeye alikuwa akiishi Bethania, kijiji cha Mariamu na Martha dada yake. (Huyu Mariamu, ambaye Lazaro kaka yake alikuwa mgonjwa, ndiye alimpaka Bwana Isa mafuta na kuifuta miguu yake kwa nywele zake.) Hivyo hawa dada wawili walituma ujumbe kwa Isa kumwambia, “Bwana, yule umpendaye ni mgonjwa.” Lakini Isa aliposikia hayo, akasema, “Ugonjwa huu hautaleta mauti, bali ni wa kudhihirisha utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu apate kutukuzwa kutokana na ugonjwa huu.” Isa aliwapenda Martha, Mariamu na Lazaro ndugu yao. Hata hivyo, baada ya kusikia kwamba Lazaro ni mgonjwa, alikawia huko alikokuwa kwa siku mbili zaidi. Ndipo akawaambia wanafunzi wake, “Haya, turudi Yudea.” Wanafunzi wake wakamwambia, “Mwalimu, Wayahudi walikuwa wanataka kukupiga mawe, nawe unataka kurudi huko?” Isa akawajibu, “Si kuna saa kumi na mbili za mchana katika siku moja? Wanaotembea mchana hawawezi kujikwaa, kwa maana wanaona kwa nuru ya ulimwengu huu. Lakini wale wanaotembea usiku hujikwaa kwa sababu hawana nuru ndani yao.” Baada ya kusema haya, Isa akawaambia, “Rafiki yetu Lazaro amelala, lakini naenda kumwamsha.” Wanafunzi wakamwambia, “Bwana, kama amelala usingizi ataamka.” Hata hivyo, Isa alikuwa anazungumzia kuwa Lazaro amekufa, lakini wanafunzi wake hawakuelewa, walidhani kwamba anasema Lazaro amelala usingizi tu. Kwa hiyo Isa akawaambia waziwazi, “Lazaro amekufa. Hata hivyo nafurahi kwa kuwa sikuwako huko kabla ya Lazaro kufa, ili mpate kuamini. Lakini sasa twendeni kwake.” Tomaso (aliyeitwa Pacha) akawaambia wanafunzi wenzake, “Sisi nasi twendeni tukafe pamoja naye.” Isa alipowasili huko alikuta Lazaro amekuwa kaburini siku nne. Basi Bethania ulikuwa karibu na Yerusalemu, umbali wa yamkini maili mbili, na Wayahudi wengi walikuwa wamekuja kuwafariji Martha na Mariamu kwa ajili ya kufiwa na ndugu yao. Martha aliposikia kwamba Isa anakuja, alitoka kwenda kumlaki, ila Mariamu alibaki nyumbani. Martha akamwambia Isa, “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa. Lakini sasa ninajua kuwa chochote utakachomwomba Mungu, atakupa.” Isa akamwambia, “Ndugu yako atafufuka.” Martha akamjibu, “Ninajua ya kuwa atafufuka wakati wa ufufuo wa wafu siku ya mwisho.” Isa akamwambia, “Mimi ndiye huo ufufuo na uzima. Yeye aniaminiye mimi, hata akifa atakuwa anaishi; na yeyote aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je, unasadiki haya?” Martha akamwambia, “Ndiyo Bwana, ninaamini ya kuwa wewe ndiwe Al-Masihi, Mwana wa Mungu, yeye ajaye ulimwenguni.” Baada ya kusema haya, Martha alienda akamwita Mariamu dada yake faraghani na kumwambia, “Mwalimu yuko hapa anakuita.” Mariamu aliposikia hivyo, akaondoka upesi, akaenda hadi alipokuwa Isa. Isa alikuwa hajaingia kijijini, bali alikuwa bado yuko mahali pale alipokutana na Martha. Wale Wayahudi waliokuwa pamoja na Mariamu nyumbani wakimfariji walipoona ameondoka haraka na kutoka nje, walimfuata wakidhani kwamba alikuwa anaenda kule kaburini kulilia huko. Mariamu alipofika mahali pale Isa alipokuwa, alipiga magoti miguuni pake na kusema, “Bwana, kama ungekuwa hapa, ndugu yangu hangekufa.” Isa alipomwona Mariamu akilia na wale Wayahudi waliokuja pamoja naye pia wakilia, Isa alisikia uchungu moyoni, akafadhaika sana. Akauliza, “Mmemweka wapi?” Wakamwambia, “Bwana, njoo upaone.” Isa akalia machozi. Ndipo Wayahudi wakasema, “Tazama jinsi alivyompenda Lazaro!” Lakini wengine wakasema, “Je, yule aliyefungua macho ya kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife?” Isa akafika penye kaburi akiwa amefadhaika sana kwa mara nyingine. Hilo kaburi lilikuwa pango ambalo jiwe liliwekwa kwenye ingilio lake. Isa akasema, “Liondoeni jiwe.” Martha dada yake yule aliyekuwa amekufa akasema, “Lakini Bwana, wakati huu atakuwa ananuka kwani amekwisha kuwa kaburini siku nne.” Isa akamwambia, “Sikukuambia kwamba ukiamini utauona utukufu wa Mungu?” Kwa hiyo wakaliondoa lile jiwe kutoka kaburini. Isa akainua macho yake juu, akasema, “Baba, ninakushukuru kwa kuwa wanisikia. Ninajua ya kuwa wewe hunisikia siku zote, lakini nimesema haya kwa ajili ya watu hawa waliosimama hapa, ili wapate kuamini ya kuwa wewe umenituma.” Baada ya kusema haya, Isa akapaza sauti yake, akaita, “Lazaro, njoo huku!” Yule aliyekuwa amekufa akatoka nje, mikono yake na miguu yake ikiwa imeviringishiwa vitambaa vya kitani na leso usoni pake. Isa akawaambia, “Mfungueni; mwacheni aende zake.” Hivyo Wayahudi wengi waliokuwa wamekuja kumfariji Mariamu walipoona yale Isa aliyoyatenda, wakamwamini.