Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Mika 6

6
Shtaka la Mwenyezi Mungu dhidi ya Israeli
1Sikiliza asemalo Mwenyezi Mungu:
“Simama, jitetee mbele ya milima;
vilima na visikie lile unalotaka kusema.
2“Sikilizeni, ee milima, mashtaka ya Mwenyezi Mungu,
sikilizeni, enyi misingi ya milele ya dunia.
Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ana shauri dhidi ya watu wake;
anatoa mashtaka dhidi ya Israeli.
3“Watu wangu, nimewatendea nini?
Nimewalemea kwa jinsi gani? Mnijibu.
4Nimewatoa kutoka Misri na kuwakomboa
kutoka nchi ya utumwa.
Nilimtuma Musa awaongoze,
pia Haruni na Miriamu.
5Watu wangu, kumbukeni jinsi Balaki mfalme wa Moabu
alivyofanya shauri
na kile Balaamu mwana wa Beori alichojibu.
Kumbukeni safari yenu kutoka Shitimu hadi Gilgali,
ili mfahamu matendo ya haki ya Mwenyezi Mungu.”
6Nimjie Mwenyezi Mungu na kitu gani na kusujudu
mbele za Mungu aliyetukuka?
Je, nije mbele zake na sadaka za kuteketezwa,
nije na ndama za mwaka mmoja?
7Je, Mwenyezi Mungu atafurahishwa na kondoo dume elfu,
au mito elfu kumi ya mafuta?
Je, nimtoe mzaliwa wangu wa kwanza
kwa ajili ya kosa langu,
mtoto wangu mwenyewe
kwa ajili ya dhambi ya nafsi yangu?
8Amekuonesha yaliyo mema, ee mwanadamu.
Mwenyezi Mungu anataka nini kwako?
Ila kutenda kwa haki na kupenda rehema,
na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako.
Hatia na adhabu ya Israeli
9Sikiliza! Mwenyezi Mungu anauita mji:
kulicha jina lako ni hekima:
“Tii hiyo fimbo na yeye aliyeiamuru.
10Je, bado nisahau, ee nyumba ya uovu,
hazina yako uliyopata kwa udanganyifu
na vipimo vilivyopunguka,
ambavyo vimelaaniwa?
11Je, naweza kuhukumu kuwa
mtu mwenye mizani ya udanganyifu hana hatia,
aliye na mfuko wa mawe ya kupimia ya uongo?
12Matajiri wake ni wajeuri;
watu wake ni waongo
na ndimi zao zinazungumza
kwa udanganyifu.
13Kwa hiyo, nimeanza kukuharibu,
kuwaangamiza kwa sababu ya dhambi zenu.
14Mtakula lakini hamtashiba;
tumbo zenu bado zitakuwa tupu.
Mtaweka akiba lakini hamtaokoa chochote,
kwa sababu mtakachoweka akiba
nitatoa kwa upanga.
15Mtapanda lakini hamtavuna;
mtakamua zeituni lakini
hamtatumia mafuta yake.
Mtakamua zabibu
lakini hamtakunywa hiyo divai.
16Mmezishika sheria za Omri
na matendo yote ya nyumba ya Ahabu,
tena umefuata desturi zao.
Kwa hiyo nitakutoa kwa maangamizi
na watu wako kuwa dhihaka;
mtachukua dharau za mataifa.”

Iliyochaguliwa sasa

Mika 6: NENO

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia