3
Hakuna tumaini katika mwili
1Hatimaye, ndugu zangu, furahini katika Bwana Isa! Mimi kuwaandikia mambo yale yale hakuniudhi, kwa maana ni kinga kwa ajili yenu.
2Jihadharini na mbwa, wale watenda maovu, jihadharini na wale wajikatao miili yao. 3Kwa maana sisi ndio tulio tohara, sisi tumwabuduo Mungu katika Roho wake Mtakatifu, tunaona fahari katika Al-Masihi Isa, ambao hatuweki tumaini letu katika mwili, 4ingawa mimi mwenyewe ninazo sababu za kuutumainia mwili.
Kama mtu yeyote akidhani anazo sababu za kuutumainia mwili, mimi zaidi. 5Nilitahiriwa siku ya nane, mimi ni Mwisraeli wa kabila la Benyamini, Mwebrania wa Waebrania. Kwa habari ya Torati, ni Farisayo#3:5 Kundi la kidini la Wayahudi; walifuata Torati kwa dhati, hasa maagizo kuhusu utakaso. Pia waliamini katika malaika, ufufuo wa wafu, na kuja kwa Masihi ambaye atarejesha ufalme wa Daudi na ukuu wa taifa la Israeli., 6kwa habari ya juhudi, nilikuwa nikitesa jumuiya ya waumini, kuhusu haki inayopatikana kwa Torati, sikuwa na hatia.
7Lakini mambo yale yaliyokuwa faida kwangu, sasa nayahesabu kuwa hasara kwa ajili ya Al-Masihi. 8Zaidi ya hayo, nayahesabu mambo yote kuwa hasara tupu nikiyalinganisha na faida kubwa ipitayo kiasi cha kumjua Al-Masihi Isa Bwana wangu, ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote, nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nimpate Al-Masihi. 9Nami nionekane mbele zake bila kuwa na haki yangu mwenyewe inayopatikana kwa sheria, bali ile inayopatikana kwa imani katika Al-Masihi, haki ile inayotoka kwa Mungu kupitia kwa imani. 10Nataka nimjue Al-Masihi na uweza wa kufufuka kwake na ushirika wa mateso yake, ili nifanane naye katika mauti yake, 11ili kwa njia yoyote niweze kufikia ufufuo wa wafu.
Kukaza mwendo ili kufikia lengo
12Si kwamba nimekwisha kufikia, au kwamba nimekwisha kuwa mkamilifu, la hasha! Bali nakaza mwendo ili nipate kile ambacho kwa ajili yake, nimeshikwa na Al-Masihi Isa. 13Ndugu zangu, sijihesabu kuwa nimekwisha kushika. Lakini ninafanya jambo moja: Ninasahau mambo yale yaliyopita, nakaza mwendo kufikia yale yaliyo mbele. 14Nakaza mwendo nifikie ile alama ya ushindi iliyowekwa ili nipate tuzo ya mwito mkuu wa Mungu ambao nimeitiwa huko juu mbinguni katika Al-Masihi Isa.
15Hivyo sisi sote tuliokuwa kiroho tuwaze jambo hili, hata mkiwaza mengine katika jambo lolote, Mungu ataliweka wazi hilo nalo. 16Lakini na tushike sana lile ambalo tumekwisha kulifikia.
17Ndugu zangu, kwa pamoja fuateni mfano wangu na kuwatazama wale wanaofuata kielelezo tulichowawekea. 18Kwa maana, kama nilivyokwisha kuwaambia mara nyingi kabla, nami sasa nasema tena hata kwa machozi, watu wengi wanaishi kama adui wa msalaba wa Al-Masihi. 19Mwisho wa watu hao ni maangamizi, mungu wao ni tumbo, na utukufu wao ni aibu, na mawazo yao yamo katika mambo ya dunia. 20Lakini uenyeji wetu uko mbinguni. Nasi tunamngoja kwa shauku Mwokozi kutoka huko, yaani Bwana Isa Al-Masihi, 21atakayeubadili mwili wetu wa unyonge, ili upate kufanana na mwili wake wa utukufu, kwa uweza ule ambao kwa huo aweza hata kuvitiisha vitu vyote chini yake.