Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Ayubu 9

9
Ayubu ajibu: Hakuna mpatanishi
1Ndipo Ayubu akajibu, na kusema,
2 # Ayu 4:17; Zab 143:2; Rum 3:20 Kweli najua kuwa ndivyo hivyo;
Lakini mtu huwaje mwenye haki mbele za Mungu?
3Kama akipenda kushindana naye,
Hawezi kumjibu neno moja katika elfu.
4Yeye ni mwenye hekima moyoni, na mwenye uwezo katika nguvu;
Ni nani aliyejifanya kuwa mgumu juu yake, naye akafanikiwa?
5Aiondoaye milima, nayo haina habari,
Akiipindua katika hasira zake.
6 # Isa 2:19-21; Hag 2:6,21; Ebr 12:26 Aitikisaye dunia itoke mahali pake,
Na nguzo zake hutetemeka.
7Aliamuruye jua, nalo halichomozi;
Nazo nyota huzipiga mhuri.
8Ambaye peke yake ni mwenye kuzitandika mbingu,
Na kuyakanyaga mawimbi ya bahari.
9 # Ayu 38:31; Amo 5:8; Mwa 1:16 Yeye afanyaye hizo nyota za Dubu, na Orioni, na hicho Kilimia,
Na makundi ya nyota ya kusini.
10Atendaye mambo makuu yasiyochunguzika;
Naam, mambo ya ajabu yasiyohesabika.
11 # Ayu 23:8 Tazama, yuaenda karibu nami, nisimwone;
Tena yuapita kwenda mbele, nisimtambue.
12 # Isa 45:9; Yer 18:6 Tazama, yuanyakua, ni nani awezaye kumzuia?
Ni nani awezaye kumwuliza, Wafanya nini?
13Mungu haondoi hasira zake;
Hao wamsaidiao Rahabu huinama chini yake.
14Je! Mimi nitamjibuje,
Na kuyachagua maneno yangu kuhojiana naye?
15 # Ayu 10:15 Ambaye, nijapokuwa mimi ni mwenye haki, siwezi kumjibu;
Ni lazima nimwombe mshitaki wangu anihurumie.
16Kama ningemwita, naye akaniitikia;
Hata hivyo singeamini kuwa amesikiza sauti yangu.
17 # Ayu 2:3; Zab 25:3; Yn 9:3 Yeye anipondaye kwa dhoruba,
Na kuyaongeza majeraha yangu pasipokuwa na sababu.
18Haniachi nipate kuvuta pumzi,
Lakini hunijaza uchungu.
19Kama tukitaja nguvu za mashujaa, tazama yupo hapo!
Kama tukitaja hukumu, ni nani atakayemwita mahakamani?
20Ingawa mimi ni mwenye haki, kinywa changu mwenyewe kitanihukumu;
Ingawa mimi ni mkamilifu, kitanishuhudia kuwa mimi ni mpotovu.
21Mimi ni mkamilifu; siangalii nafsi yangu;
Naudharau uhai wangu.
22 # Mhu 9:1,2; Eze 21:3; Lk 13:2-4 Hayo yote ni mamoja; kwa hiyo nasema,
Yeye huangamiza wakamilifu na waovu pia.
23Kama hilo pigo likiua ghafla,
Atayadhihaki majaribu yake asiye na kosa.
24 # 2 Sam 15:30; Yer 14:4 Dunia imetiwa mkononi mwa waovu;
Yeye hufunika nyuso za waamuzi wake;
Kama si yeye, ni nani basi?
25Basi siku zangu zina mbio kuliko tarishi;
Zakimbia, wala hazioni mema.
26Zimepita kama merikebu ziendazo mbio;
Mfano wa tai ayashukiaye mawindo.
27Nikisema, Mimi nitasahau kuugua kwangu,
Nitaacha kununa uso nikachangamke moyo;
28 # Kut 20:7; Zab 130:3 Mimi ninayaogopa mateso yangu yote,
Najua kuwa hutanihesabu kuwa sina hatia.
29Nitahukumiwa kuwa ni mkosa;
Ya nini basi nitaabike bure?
30Ingawaje najiosha kwa maji ya theluji,
Na kuitakasa mikono yangu kwa sabuni;
31Lakini utanitupa shimoni,
Nami hata nguo zangu zitanichukia.
32 # Mhu 6:10; Isa 45:9; Yer 49:19 Maana yeye si mtu, kama mimi, hata nimjibu,
Hata tuwe mahakamani pamoja.
33 # 1 Sam 2:25 Hapana mwenye kuamua katikati yetu,
Awezaye kutuwekea mkono sote wawili.
34Na aniondolee fimbo yake,
Na utisho wake usinitie hofu;
35Hapo Ndipo ningeweza kusema, pasipo kumwogopa;
Maana najua sivyo nilivyo nafsini mwangu.

Iliyochaguliwa sasa

Ayubu 9: SRUV

Kuonyesha

Shirikisha

Nakili

None

Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia