Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Zekaria 13:1-9

Zekaria 13:1-9 SRUV

Katika siku hiyo watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, watafunguliwa chemchemi ya kuwatakasa kutoka kwa dhambi na kwa unajisi. Kisha itakuwa katika siku hiyo, asema BWANA wa majeshi, nitakatilia mbali majina ya sanamu katika nchi, yasikumbukwe tena; pia nitawafukuza manabii, na roho ya uchafu, watoke katika nchi. Tena itakuwa ya kwamba, mtu awaye yote atakapotoa unabii, basi baba yake na mama yake waliomzaa watamwambia, Hutaishi; kwa maana unanena maneno ya uongo kwa jina la BWANA; na baba yake na mama yake waliomzaa watamtumbua atoapo unabii. Tena itakuwa siku hiyo, ya kwamba manabii, kila mmoja wao, atayaonea haya maono yake atoapo unabii; wala hawatavaa joho la nywele ili kudanganya watu; bali atasema, Mimi si nabii kamwe; mimi ni mkulima wa nchi; kwa maana nilifanywa mtumwa tokea ujana wangu. Na mtu yeyote akimwuliza, Je! Majeraha haya yote uliyo nayo katikati ya mikono yako ni nini? Naye atajibu, Ni majeraha niliyotiwa katika nyumba ya rafiki zangu. Amka, Ee upanga, juu ya mchungaji wangu, na juu ya mtu aliye mwenzangu, asema BWANA wa majeshi; mpige mchungaji, nao kondoo watatawanyika; nami nitaugeuza mkono wangu juu ya wadogo. Hata itakuwa, ya kwamba katika nchi yote mafungu mawili yatakatiliwa mbali, nao watakufa, asema BWANA; lakini fungu la tatu litabaki humo. Nami nitalileta fungu lile la tatu na kulipitisha kati ya moto, nami nitawasafisha kama fedha isafishwavyo, nami nitawajaribu kama dhahabu ijaribiwavyo; wataliitia jina langu, nami nitawasikia; mimi nitasema, Watu hawa ndio wangu; nao watasema, BWANA ndiye Mungu wangu.

Soma Zekaria 13

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na Zekaria 13:1-9