Danieli UTANGULIZI
UTANGULIZI
Mtu anayehusika sana katika kitabu hiki ni Danieli, mmoja wa wale watu waliopelekwa uhamishoni Babuloni katika mwaka wa 597 K.K.
Lengo la mwandishi ni kuwatuliza watu. Anataka kuwapa watu matumaini kwamba Mungu atawaangamiza wadhalimu na kuwaweka huru na salama wale wanaodhulumiwa na kuonewa. Kitabu kinatia mkazo jambo la kuwa imara katika imani na kwamba watu wanaobaki wakimtegemea Mungu watakombolewa. Danieli ni kielelezo cha kuwa na imani thabiti.
Kitabu chenyewe kwa muundo wake na namna yake ya kueleza mambo ni mojawapo ya vile vitabu kadhaa vya Biblia vinavyojulikana kama vya maandishi yahusuyo “Mambo ya Mwisho” au “Apokaliptiki.” Maandishi ya namna hiyo yanazungumzia kuangamizwa kwa tawala za mabavu duniani na kuanzishwa kwa utawala wa Mungu. Jambo hilo laelezwa mara nyingi kwa njia ya vielelezo na maono mbalimbali. Ufasaha au namna hiyo ya maandishi yatokea pia katika Isaya 24–27, katika sehemu ya Yoeli na Zekaria, na katika Kitabu cha Ufunuo katika Agano Jipya.
Kitabu cha Danieli ni tofauti na vitabu vya manabii, na katika orodha ya vitabu katika Biblia ya Kiebrania kitabu cha Danieli hakimo katika fungu la vitabu vya manabii, bali kimeorodheshwa pamoja na vitabu vilivyojulikana kama “Maandishi.” Tazama pia utangulizi wa Agano la Kale.
Sehemu mbili zabainishwa katika kitabu hiki:
Sura 1–6. Simulizi juu ya mambo yaliyowapata Danieli na rafiki zake. Waliokolewa kutoka kwenye mikasa mbalimbali ya taabu kwa sababu ya tegemeo lao kwa Mungu na utii wao uliolingana na imani yao.
Sura 7–12. Sehemu hii inatupa maono kadha wa kadha ya Danieli ambamo tawala kadhaa za ulimwengu wa nyakati hizo zinahusika: Babuloni, Medi, Persia na Ugiriki. Maono yote yanaelezwa kwa mifano na vielelezo.
Iliyochaguliwa sasa
Danieli UTANGULIZI: BHN
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Biblia Habari Njema kwa Watu Wote (Yenye Vitabu vya Deuterokanoni): Tafsiri ya Ushirikiano wa Makanisa (BHN): Hakimiliki -1995, 2001: kwa Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.