Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Waebrania 1:5-14

Waebrania 1:5-14 BHN

Maana Mungu hakumwambia kamwe hata mmoja wa malaika wake: “Wewe ni Mwanangu; mimi leo nimekuwa Baba yako.” Wala hakusema juu ya malaika yeyote: “Mimi nitakuwa Baba yake, naye atakuwa Mwanangu.” Lakini Mungu alipokuwa anamtuma Mwanae, mzaliwa wa kwanza, ulimwenguni alisema: “Malaika wote wa Mungu na wamwabudu.” Lakini kuhusu malaika, alisema: “Amewafanya malaika wake kuwa upepo, na wahudumu wake ndimi za moto.” Lakini kuhusu Mwana, Mungu alisema: “Kiti chako cha enzi, ee Mungu, chadumu milele na milele! Wewe wawatawala watu wako kwa haki. Wewe wapenda uadilifu na kuchukia uovu. Ndiyo maana Mungu, Mungu wako, amekuweka wakfu na kukumiminia furaha kubwa kuliko wenzako.” Na tena: “Bwana, wewe uliumba dunia hapo mwanzo, mbingu ni kazi ya mikono yako. Hizo zitatoweka, lakini wewe wabaki daima, zote zitachakaa kama vazi. Utazikunjakunja kama koti, nazo zitabadilishwa kama vazi. Lakini wewe ni yuleyule daima, na maisha yako hayatakoma.” Mungu hakumwambia kamwe hata mmoja wa malaika wake: “Keti upande wangu wa kulia, mpaka niwaweke adui zako chini ya miguu yako.” Malaika ni nini ila roho wanaomtumikia Mungu na ambao hutumwa kuwasaidia wale watakaopokea wokovu?