Matendo ya Mitume 11
11
Maelezo ya Petro kwa kanisa la Yerusalema
1Mitume na wandugu waamini waliokuwa Yudea wakasikia kwamba watu wamoja wa mataifa mengine wameamini Neno la Mungu vilevile. 2Na Petro aliporudi Yerusalema, wale wanafunzi Wayuda wakabishana naye, 3wakisema: “Uliingia ndani ya nyumba ya watu wasiokuwa wa taifa letu na kula chakula pamoja nao!”
4Halafu Petro akaanza kuwaelezea mambo yote yaliyotokea kwa utaratibu. Akawaambia: 5“Mimi nilikuwa katika muji Yopa nikiomba. Kisha nikakuwa sawa nimezimia, nami nikapata maono. Nikaona kitu kinachokuwa kama nguo kubwa kikishuka toka mbingu, kikitelemushwa, kikishikwa kwenye pembe zake ine. Nacho kikafika karibu nami. 6Nilipochungulia ndani yake kwa uangalifu, nikaona nyama wa ufugo wenye miguu mine, nyama wa pori, nao nyama wenye kutambaa pamoja na ndege. 7Na nikasikia sauti ikiniambia: ‘Petro, simama. Chinja na ukule!’ 8Lakini nikajibu: ‘Hapana, hata kidogo, ee Bwana! Ndani ya kinywa changu hamujaingia bado kitu chochote kisichoruhusiwa kukuliwa wala chochote kinachohesabiwa kuwa kichafu.’ 9Lakini sauti ikanirudilia kutoka mbingu ikisema: ‘Vitu vilivyotakaswa na Mungu, usivihesabu kuwa vichafu.’ 10Nayo maneno haya yakasikilika tena mara tatu, kisha vile vitu vyote vikanyanyuliwa mbinguni. 11Na saa ile ile watu watatu waliotumwa kwangu kutoka muji Kaisaria wakafika kwa mulango wa nyumba niliyokaa ndani yake. 12Naye Roho Mutakatifu akaniambia kwamba niende pamoja nao bila kusita. Na hawa wandugu sita munaowaona wakanisindikiza, nasi tukafika na kuingia sisi wote ndani ya nyumba ya Kornelio. 13Naye akatuelezea namna malaika alivyomutokea ndani ya nyumba yake na kumwambia: ‘Tuma wajumbe, kwenda Yopa kwa kumwita Simoni, anayeitwa vilevile Petro. 14Ni yeye atakayekuambia mambo yanayokupasa wewe pamoja na watu wote wa nyumba yako kusudi mupate kuokolewa.’ 15Nami nilipoanza kusema, Roho Mutakatifu akashuka juu yao sawa vile alivyoshuka juu yetu kwanza. 16Halafu nikakumbuka maneno haya Bwana aliyosema: ‘Yoane amebatiza kwa maji, lakini ninyi mutabatizwa kwa Roho Mutakatifu.’ 17Basi ikiwa Mungu aliwapa wale watu zawadi ile ile Roho Mutakatifu aliyotupatia sisi wakati tulipomwamini Bwana Yesu Kristo, mimi ni nani hata nisubutu kupingana na Mungu?”
18Wandugu waamini waliposikia maneno hayo, wakatulia na kumusifu Mungu, wakisema: “Kumbe Mungu amewajalia hata watu wa mataifa mengine vilevile kusudi waweze kugeuka toka zambi na kupata uzima kamili.”
Mwanzo wa kanisa la Antiokia
19Nyuma ya kuuawa kwa Stefano, wanafunzi walisambaa kwa ajili ya mateso. Nao wakasafiri mpaka katika inchi ya Foinikia na ya Kipuro na kufika katika muji Antiokia. Na kule walihubiri Neno la Mungu, lakini kwa Wayuda peke yao tu. 20Lakini kulitokea wanafunzi wengine, waliokuwa watu wa Kipuro na wa inchi ya Kurene, waliofika Antiokia. Nao wakaanza kusemezana na Wagriki vilevile, wakiwahubiri Habari Njema juu ya Bwana Yesu. 21Na Bwana akawaongoza kwa uwezo wake, hata watu wengi sana wakaamini neno la Bwana na kumugeukia.
22Watu wa kanisa la Yerusalema waliposikia habari hii, wakamutuma Barnaba kwenda kule Antiokia. 23Naye alipofika, akaona mambo yote yaliyotendeka kutokana na neema ya Mungu, akafurahi, naye akawatia wanafunzi wote moyo kusudi waendelee kushikamana na Bwana kwa moyo wao wote. 24Barnaba alikuwa mutu mwema, mwenye kujazwa na Roho Mutakatifu na mwenye imani sana. Na watu wengi wakaongezeka kwa Bwana.
25Kisha Barnaba akatoka kule na kwenda Tarso kwa kumutafuta Saulo. 26Naye alipomwona, akamuleta Antiokia. Na kwa muda wa mwaka muzima Barnaba na Saulo walikusanyika katika kanisa la kule na wakawafundisha watu wengi. Ni kule Antiokia ndiko wanafunzi waliitwa kwa mara ya kwanza jina la Wakristo.
27Katika siku zile, manabii wamoja walifika Antiokia wakitoka Yerusalema. 28Na mumoja wao, aliyeitwa Agabo, akasimama, akatabiri kwa njia ya Roho Mutakatifu kwamba kutakuwa njaa kubwa katika dunia nzima. (Nayo ikatokea katika nyakati za utawala wa mufalme Klaudio wa Roma.) 29Wanafunzi wakakusudia kutuma musaada kwa wandugu waamini waliokaa katika jimbo la Yudea, kila mumoja kwa kadiri alivyoweza kutoa. 30Nao wakafanya vile, wakatuma misaada waliyokusanya kwa wazee wa kanisa kwa mukono wa Barnaba na Saulo.
Currently Selected:
Matendo ya Mitume 11: SWC02
Highlight
Share
Copy
Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.