YouVersion Logo
Search Icon

Matendo ya Mitume 8

8
1Naye Saulo alikuwa amekubali kwamba Stefano anastahili kuuawa.
Saulo anatesa kanisa
Siku ile ile kanisa lililokuwa katika Yerusalema lilianza kupata mateso makubwa. Waamini wote walisambaa katika Yudea na Samaria, isipokuwa mitume tu. 2Watu wenye kuogopa Mungu wakamuzika Stefano na kumufanyia kilio kikubwa.
3Lakini Saulo aliendelea kuteketeza kanisa, akiingia nyumba kwa nyumba, na kuwakamata waamini, wanaume na wanawake, na kwenda kuwatupa katika kifungo.
Filipo anahubiri katika Samaria
4Wale waamini waliosambaa walikwenda popote wakitangaza Habari Njema. 5Naye Filipo akaenda katika muji mukubwa wa Samaria na kuwahubiri wakaaji wake juu ya Kristo. 6Makundi ya watu waliposikia maneno yale Filipo aliyosema na kuona vitambulisho alivyoonyesha, wote walimusikiliza kwa nia moja na kwa uangalifu. 7Maana pepo walitoka ndani ya watu wengi wakilalamika kwa sauti kubwa, na watu wengi wenye kupooza pamoja na viwete waliponyeshwa vilevile. 8Hivi kukakuwa furaha kubwa katika muji ule.
9Na kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Simoni aliyekuwa akikaa katika muji ule ule tangu mbele. Yeye alikuwa akifanya mambo ya uchawi na kuwashangaza watu wa Samaria. Alijidai kuwa yeye ni mutu mukubwa. 10Watu wote, tangia wadogo mpaka wakubwa walimusikiliza kwa uangalifu, wakisema: “Mutu huyu ndiye ule uwezo wa Mungu unaoitwa ‘Uwezo Mukubwa.’ ”
11Hakika walimusikiliza vizuri kwa sababu aliwashangaza kwa muda wa siku nyingi kwa njia ya uchawi wake. 12Lakini walipoamini Habari Njema ambayo Filipo alihubiri juu ya Ufalme wa Mungu na juu ya Yesu Kristo, wanaume na wanawake wakabatizwa. 13Hata Simoni vilevile akaamini na kubatizwa. Na nyuma ya pale alishikamana na Filipo, naye alishangaa sana alipoona kitambulisho kikubwa na miujiza iliyokuwa ikifanyika.
14Mitume waliokuwa Yerusalema waliposikia kwamba wakaaji wa Samaria wamekubali Neno la Mungu, wakawatumia Petro na Yoane. 15Walipofika Samaria, wakawaombea waamini wapate kupokea Roho Mutakatifu. 16Kwa maana Roho Mutakatifu alikuwa bado hajashuka hata juu ya mumoja wao; walikuwa tu wamebatizwa kwa jina la Bwana Yesu. 17Halafu Petro na Yoane wakaweka mikono juu yao, nao wakapokea Roho Mutakatifu.
18Simoni alipoona kwamba wanafunzi wamepokea Roho Mutakatifu kwa njia ya kuwekewa mikono ya mitume, akaletea Petro na Yoane feza na kuwaambia: 19“Munipe nami vilevile uwezo huu; kusudi yeyote nitakayeweka mikono juu yake, apate kupokea Roho Mutakatifu.”
20Lakini Petro akamujibu: “Feza yako ipotelee mbali pamoja nawe, kwa sababu umezani kwamba unaweza kununua ile zawadi ya Mungu kwa njia ya feza! 21Wewe hauna sehemu wala haki yoyote katika jambo hili, kwa sababu moyo wako si mukamilifu mbele ya Mungu. 22Basi ugeuke toka katika zambi zako na umwombe Bwana, labda atakusamehe kwa ajili ya mawazo ya namna hii. 23Kwa maana ninaona kwamba umejaa uchungu sana nawe umefungwa na zambi.”
24Halafu Simoni akawaambia Petro na Yoane: “Muniombee ninyi wenyewe kwa Bwana, kusudi lisinipate hata neno moja kati ya maneno haya muliyosema.”
25Kisha kushuhudia na kuhubiri neno la Bwana, Petro na Yoane wakarudi Yerusalema wakitangaza Habari Njema katika vijiji vingi vya Samaria.
Filipo na mukubwa mumoja wa Etiopia
26Malaika wa Bwana akamwambia Filipo: “Ujitayarishe na uende upande wa kusini kupitia njia inayotelemuka toka Yerusalema kwenda katika muji Gaza, nayo ni njia watu wasiyozoea kupitia.”
27Basi Filipo akajitayarisha na kwenda. Alipokuwa katika njia, mara moja akakutana na towashi mumoja Mwetiopia. Mutu huyu alikuwa mukubwa, alishugulika na kazi ya usimamizi wa mali zote za malkia Kandake wa Etiopia. Yeye alikuwa amekwenda Yerusalema kwa kumwabudu Mungu, 28na sasa alikuwa katika safari ya kurudi kwake. Alikuwa akiikaa ndani ya gari lake akisoma katika kitabu cha nabii Isaya. 29Roho Mutakatifu akamwambia Filipo: “Endelea, usogee karibu na lile gari.”
30Filipo akaenda mbio karibu na gari, naye akamusikia yule mukubwa akisoma katika kitabu cha nabii Isaya. Filipo akamwuliza: “Unaelewa maneno unayoyasoma?”
31Naye akamujibu: “Nitayaelewa namna gani pasipo mutu wa kunielezea?”
Halafu akamwomba Filipo apande na kuikaa karibu naye ndani ya gari. 32Na sehemu ya Maandiko aliyokuwa akisoma ni hii:
“Alipelekwa kama kondoo kwenda kuchinjwa,
kama mwana-kondoo anayenyamaza mbele ya mwenye kumukata manyoya.
Yeye hakufungua kinywa chake.
33Alinyenyekezwa na kuhukumiwa bila haki.
Hakuna mutu atakayeweza kueleza habari za kizazi chake,
maana maisha yake yameondolewa katika dunia.”
34Yule mukubwa akamwuliza Filipo: “Ninakusihi uniambie, nabii huyu anasema juu ya nani? Ni juu yake mwenyewe au juu ya mutu mwingine?”
35Basi Filipo akaanza na sehemu ile ile ya maandiko, akamwelezea Habari Njema juu ya Yesu. 36Walipokuwa wakiendelea na safari, wakafika kwenye nafasi moja kwenye maji, yule mukubwa akasema: “Hapa kuna maji. Ni kitu gani kinachonizuiza nisibatizwe?”
[ 37Filipo akamwambia: “Kama unaamini kwa moyo wako wote, unaweza kubatizwa.”
Yule mukubwa akamujibu: “Ninaamini kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu.”]
38Kisha akasimamisha gari. Filipo na yule mukubwa wakashuka wote wawili ndani ya maji na Filipo akamubatiza. 39Walipotoka ndani ya maji, kwa rafla Roho wa Bwana akamutowesha Filipo, na yule mukubwa hakumwona tena, lakini akaongeza safari yake katika furaha. 40Filipo akajikuta amekwisha kuwa katika muji Azoto. Kisha akapita katika miji yote akihubiri Habari Njema, mpaka alipofika katika muji Kaisaria.

Currently Selected:

Matendo ya Mitume 8: SWC02

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

Video for Matendo ya Mitume 8