YouVersion Logo
Search Icon

Matendo ya Mitume 9

9
Kugeuka kwa Saulo
(Mdo 22.6-16; 26.12-18)
1Katika siku zile zile, Saulo aliendelea na vitisho vikali vya kuwaua wanafunzi wa Bwana. Siku moja akamwendea Kuhani Mukubwa 2na kumwomba amwandikie barua za kumutambulisha katika nyumba za kuabudia za muji Damasiki. Katika barua hizo, Saulo alipewa ruhusa kwamba akiona watu wanaofuata Njia ya Bwana, ikiwa wanaume au wanawake, awafunge na kuwapeleka Yerusalema.
3Alipokuwa katika safari karibu kufika Damasiki, kwa rafla mwangaza toka mbinguni ukamuzunguka. 4Akaanguka chini, akasikia sauti ikimwambia: “Saulo, Saulo, sababu gani unanitesa?”
5Naye akauliza: “Wewe ni nani, Bwana?”
Na Bwana akajibu: “Mimi ni Yesu unayemutesa. 6Lakini simama, uingie katika muji, na mule watakuambia jambo unalopaswa kufanya.”
7Nao watu waliosafiri pamoja na Saulo wakasimama na kubaki kimya kwa ajili ya mushangao, kwa maana walisikia sauti lakini hawakuona mutu. 8Saulo akasimama wima, na ingawa macho yake yalikuwa wazi hakuweza kuona kitu. Halafu wakamushika mukono na kumwongoza mpaka ndani ya muji Damasiki. 9Akabaki muda wa siku tatu pasipo kuona, naye hakukula wala kunywa kitu.
10Na kule Damasiki kulikuwa mwanafunzi mumoja wa Yesu jina lake Anania. Bwana akamutokea katika maono, akamwita akisema: “Anania!”
Naye akamwitikia, akisema: “Bwana, mimi niko hapa.”
11Bwana akamwambia: “Kwenda katika barabara wanayoita ‘Yenye Kunyooka,’ uingie ndani ya nyumba ya Yuda, na mule umutafute mutu wa muji wa Tarso anayeitwa Saulo, utamukuta akiomba. 12Yeye ameona katika maono mutu mumoja anayeitwa Anania, akiingia ndani ya nyumba na kuweka mikono juu yake kusudi apate kuona tena.”
13Anania akajibu: “Bwana, nimekwisha kusikia watu wengi wakisema habari za mutu huyo, wakieleza mabaya aliyowatendea watu wako watakatifu wanaokuwa Yerusalema. 14Na hata huku yuko na mamlaka aliyopewa na wakubwa wa makuhani kusudi afunge wote wanaoomba kwa jina lako.”
15Lakini Bwana akamwambia: “Kwenda tu, kwa maana nimemuchagua mutu huyu kwa kunitumikia, kusudi atangaze jina langu kwa mataifa, kwa wafalme na kwa Waisraeli. 16Nami nitamwonyesha mateso ya namna gani atakayopaswa kupata kwa ajili yangu.”
17Basi Anania akaenda. Alipofika ndani ya nyumba ambamo Saulo alikuwa, akaweka mikono juu yake na kumwambia: “Ndugu Saulo, Bwana Yesu aliyekutokea katika njia ulipokuwa ukikuja huku, amenituma kusudi upate kuona tena na kujazwa na Roho Mutakatifu.”
18Na pale pale vitu vilivyokuwa kama magamba vikaanguka toka ndani ya macho ya Saulo, naye akapata tena kuona. Halafu akasimama na kubatizwa. 19Kisha akakula chakula, na kupata nguvu tena.
Saulo anahubiri katika Damasiki
Saulo alikaa siku chache pamoja na wanafunzi waliokuwa Damasiki. 20Na bila kukawia akaanza kuhubiri katika nyumba za kuabudia, akitangaza kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu. 21Wote waliomusikia walishangaa, wakisema: “Si mutu huyu ndiye aliyewatesa vikali kule Yerusalema watu wanaoomba kwa jina la Yesu? Hakika amefika huku nako kusudi awafunge watu kama hao na kuwapeleka kwa wakubwa wa makuhani.”
22Lakini Saulo akazidi kuhubiri na uwezo, akawashinda Wayuda waliokaa Damasiki akihakikisha wazi kwao kwamba Yesu ndiye Kristo.
23Na kulipokwisha kupita siku nyingi, Wayuda wakafanya shauri la kumwua Saulo, 24lakini Saulo akavumbua shauri lile. Nao walichunga milango ya kuingilia ndani ya muji ule muchana na usiku kusudi wamwue, 25lakini siku moja usiku wanafunzi wa Saulo wakamutwaa, wakamuweka ndani ya kitunga na kumutelemusha na kamba inje ya ukuta.
Saulo anarudi katika Yerusalema
26Saulo alipofika Yerusalema, alijaribu kujiunga na wanafunzi wengine, lakini wote walimwogopa, kwa sababu hawakusadiki kwamba amekwisha kugeuka mwanafunzi. 27Basi Barnaba akamutwaa na kumupeleka kwa mitume. Akawaelezea namna Saulo alivyomwona Bwana katika njia na jinsi Bwana alivyosema naye. Akawaelezea vilevile namna Saulo alihubiri kwa jina la Yesu pasipo woga katika Damasiki. 28Saulo akakaa pamoja nao, akaenda huku na huko katika muji Yerusalema akihubiri kwa jina la Yesu pasipo woga. 29Vilevile alisemezana na kubishana na Wayuda waliosema kigriki, lakini wao walitafuta njia ya kumwua. 30Wandugu walipopata habari ile, wakamupeleka mbali katika muji Kaisaria, na kutoka kule wakamutuma aende katika muji Tarso.
31Wakati ule, kanisa lilikuwa na amani katika Yudea yote, Galilaya na Samaria. Vilevile lilizidi kupata nguvu na kuendelea kumwogopa Bwana, nalo liliongezeka kwa musaada wa Roho Mutakatifu.
Petro anaponyesha Ainea
32Petro alipokuwa akipita fasi zote katika majimbo yale, siku moja akawatembelea wanafunzi walioishi katika muji wa Luda. 33Kule akamwona mutu mumoja mwenye ugonjwa wa kupooza aliyeitwa Ainea aliyeshindwa kutoka ndani ya kitanda kwa muda wa miaka minane. 34Petro akamwambia: “Ainea, Yesu Kristo anakuponyesha. Simama, ujitandikie kitanda chako wewe mwenyewe.” Na mara moja Ainea akasimama. 35Nao wakaaji wote wa Luda na bonde la Saroni walipoona jambo hilo wakamugeukia Bwana.
Petro anamufufua Dorika
36Katika muji wa Yopa kulikuwa mwanafunzi mumoja mwanamuke aliyeitwa Tabita. (Katika kigriki ni “Dorika,” maana yake “Pongo”.) Mwanamuke huyu alikuwa akifanya matendo mengi mema na kuwasaidia wamasikini. 37Katika siku zile akapata ugonjwa, naye akakufa. Walipokwisha kunawisha maiti yake, wakailalisha ndani ya chumba cha gorofi. 38Na kwa kuwa muji Luda ulikuwa karibu na muji Yopa, wanafunzi walikuwa wamesikia kwamba Petro yuko kule. Kwa hiyo wakatuma kwake wajumbe wawili kwa kumwambia: “Tunakusihi, ufike huku kwetu bila kukawia.” 39Mara moja Petro akaenda pamoja nao. Naye alipofika wakamupeleka ndani ya chumba cha gorofi. Wajane wote wakamuzunguka Petro, wakilia na kumwonyesha kanzu na nguo zote Dorika alizowashonea wakati alipokuwa angali muzima. 40Petro akawaamuru watu wote waende inje, akapiga magoti na kuomba. Kisha akaelekea ile maiti na kusema: “Tabita, simama!”
Halafu Tabita akafungua macho, na wakati alipomwona Petro akaamuka na kuikaa. 41Petro akamushika mukono na kumusimamisha wima. Kisha akawaita wanafunzi na wajane, akamupeleka mbele yao akiwa muzima. 42Na habari hii ikaenea katika muji wote wa Yopa, kwa hiyo watu wengi wakamwamini Bwana. 43Petro akakaa siku nyingi huko Yopa kwa fundi mumoja wa kutengeneza vitu vya ngozi, aliyeitwa Simoni.

Currently Selected:

Matendo ya Mitume 9: SWC02

Highlight

Share

Copy

None

Want to have your highlights saved across all your devices? Sign up or sign in

Video for Matendo ya Mitume 9