Mhubiri 8
8
1Ni nani aliye kama mtu mwenye hekima?
Ni nani ajuaye maelezo ya mambo?
Hekima hung’arisha uso wa mtu na kubadili ugumu wa uso wake.
Mtii mfalme
2Nawaambia, Tii amri ya mfalme, kwa sababu uliapa mbele za Mungu. 3Usiharakishe kuondoka mbele ya mfalme. Usiendelee kutenda lililo baya, kwa maana mfalme atafanya lolote apendalo. 4Kwa kuwa neno la mfalme ndilo lenye mamlaka ya mwisho, nani awezaye kumwambia, “Je, wewe unafanya nini?”
5Yeyote anayetii agizo lake hatadhurika,
moyo wa hekima utajua wakati mwafaka
na jinsi ya kutenda.
6Kwa maana kuna wakati mwafaka
na utaratibu wa kila jambo,
ingawa huzuni ya mwanadamu
huwa nzito juu yake.
7Kwa vile hakuna mtu ajuaye siku zijazo,
ni nani awezaye kumwambia linalokuja?
8Hakuna mwanadamu
awezaye kushikilia roho yake asife,
wala hakuna mwenye uwezo
juu ya siku ya kufa kwake.
Kama vile hakuna yeyote arudishwaye nyuma wakati wa vita,
kadhalika uovu hautawaweka huru wale wautendao.
9Yote haya niliyaona, nilipokuwa natafakari kila kitu kinachotendeka chini ya jua. Kuna wakati mtu hujifanya bwana juu ya wengine kwa madhara yake mwenyewe. 10Ndipo pia nikaona waovu wakizikwa, wale waliozoea kuingia na kutoka mahali patakatifu na kupewa sifa katika mji ambao waliyafanya haya. Hili nalo ni ubatili.
11Wakati hukumu juu ya tendo ovu haitekelezwi upesi, mioyo ya watu hujaa mipango ya kutenda maovu. 12Ingawa mtu mwovu hufanya maovu mia moja na akaendelea kuishi maisha marefu, najua kwamba itakuwa bora zaidi kwa watu wanaomwogopa Mungu, wamchao Mungu. 13Lakini kwa sababu waovu hawamwogopi Mungu, hawatafanikiwa, maisha yao hayatarefuka kama kivuli.
14Kuna kitu kingine ambacho ni ubatili kinachofanyika duniani: Watu waadilifu kupata yale yanayowastahili waovu, nao waovu kupata yale yanayowastahili waadilifu. Hili nalo pia, nasema ni ubatili. 15Kwa hiyo mimi ninasifu kufurahia maisha, kwa sababu hakuna kitu bora zaidi kwa mwanadamu chini ya jua kuliko kula, kunywa na kufurahi. Kisha furaha itafuatana naye kazini mwake siku zote za maisha yake ambazo amepewa na Mungu chini ya jua.
16Nilipotafakari akilini mwangu ili nijue hekima na kuangalia kazi ya mwanadamu duniani, jinsi macho yake hayapati usingizi mchana wala usiku, 17ndipo nikaona yale yote ambayo Mungu ameyafanya. Hakuna yeyote awezaye kuelewa yale yanayotendeka chini ya jua. Licha ya juhudi zake zote za kutafuta, mtu hawezi kugundua maana yake. Hata ingawa mtu mwenye hekima anadai kuwa anafahamu, kwa hakika hawezi kutambua.
Iliyochaguliwa sasa
Mhubiri 8: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
![None](/_next/image?url=https%3A%2F%2Fimageproxy.youversionapistaging.com%2F58%2Fhttps%3A%2F%2Fweb-assets.youversion.com%2Fapp-icons%2Fsw.png&w=128&q=75)
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.