Mika 3
3
Viongozi na manabii wakemewa
1Kisha nikasema,
“Sikilizeni enyi viongozi wa Yakobo,
enyi watawala wa nyumba ya Israeli.
Je, hampaswi kujua hukumu,
2ninyi mnaochukia mema
na kupenda maovu;
ninyi mnaowachuna watu wangu ngozi
na kuondoa nyama kwenye mifupa yao;
3ninyi mnaokula nyama ya watu wangu,
mnaowachuna ngozi
na kuvunja mifupa yao vipande vipande;
mnaowakatakata kama nyama
ya kuwekwa kwenye sufuria
na kama nyama
ya kuwekwa kwenye chungu?”
4Kisha watamlilia Mwenyezi Mungu,
lakini hatawajibu.
Wakati huo atawaficha uso wake
kwa sababu ya uovu waliotenda.
5Hili ndilo asemalo Mwenyezi Mungu:
“Kuhusu manabii wanaowapotosha watu wangu,
mtu akiwalisha,
wanatangaza ‘amani’;
kama hakufanya hivyo,
wanaandaa kupigana vita dhidi yake.
6Kwa hiyo usiku utawajieni, msiweze kuwa na maono,
na giza, msiweze kubashiri.
Jua litawachwea manabii hao,
nao mchana utakuwa giza kwao.
7Waonaji wataaibika
na waaguzi watafedheheka.
Wote watafunika nyuso zao
kwa sababu hakuna jibu litokalo kwa Mungu.”
8Lakini mimi nimejazwa nguvu,
nimejazwa Roho wa Mwenyezi Mungu,
haki na uweza,
kumtangazia Yakobo kosa lake,
na Israeli dhambi yake.
9Sikieni hili, enyi viongozi wa nyumba ya Yakobo,
enyi watawala wa nyumba ya Israeli,
mnaodharau haki
na kupotosha kila lililo sawa;
10mnaojenga Sayuni kwa kumwaga damu
na Yerusalemu kwa uovu.
11Viongozi wake wanahukumu kwa rushwa,
na makuhani wake wanafundisha kwa malipo,
nao manabii wake wanatabiri kwa fedha.
Hata hivyo wanamwegemea Mwenyezi Mungu na kusema,
“Je, Mwenyezi Mungu si yumo miongoni mwetu?
Hakuna maafa yatakayotupata.”
12Kwa ajili yenu,
Sayuni italimwa kama shamba,
Yerusalemu itakuwa lundo la kokoto,
na kilima cha Hekalu
kitakuwa kichuguu
kilichofunikwa na vichaka.
Iliyochaguliwa sasa
Mika 3: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
![None](/_next/image?url=https%3A%2F%2Fimageproxy.youversionapistaging.com%2F58%2Fhttps%3A%2F%2Fweb-assets.youversion.com%2Fapp-icons%2Fsw.png&w=128&q=75)
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.