Zaburi 31
31
Zaburi 31
Maombi na sifa kwa kuokolewa kutoka kwa adui
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
1Ee Mwenyezi Mungu, nimekukimbilia wewe,
usiache nikaaibika kamwe,
kwa haki yako uniokoe.
2Nitegee sikio lako,
uje uniokoe haraka;
uwe kwangu mwamba wa kimbilio,
ngome imara ya kuniokoa.
3Kwa kuwa wewe ni mwamba wangu na ngome yangu,
uniongoze na kunilinda kwa ajili ya jina lako.
4Uniepushe na mtego niliotegewa,
maana wewe ndiwe kimbilio langu.
5Ninaikabidhi roho yangu mikononi mwako,
unikomboe Ee Mwenyezi Mungu, uliye Mungu wa kweli.
6Ninawachukia wale wanaoshikilia sanamu batili;
bali mimi ninamtumaini Mwenyezi Mungu.
7Nitafurahia na kushangilia upendo wako,
kwa kuwa uliona mateso yangu
na ulijua maumivu ya nafsi yangu.
8Hukunikabidhi kwa adui yangu
bali umeiweka miguu yangu mahali penye nafasi.
9Ee Mwenyezi Mungu unihurumie, kwa kuwa niko kwenye shida;
macho yangu yanafifia kwa huzuni,
nafsi yangu na mwili wangu kwa sikitiko.
10Maisha yangu yamedhoofika kwa majonzi,
naam, miaka yangu kwa kulia kwa maumivu makali;
nguvu zangu zinaisha kwa ajili ya mateso,
na mifupa yangu inachakaa.
11Kwa sababu ya adui zangu wote,
nimedharauliwa kabisa na majirani zangu,
hata kwa rafiki zangu nimekuwa tisho,
wale wanaoniona barabarani wananikimbia.
12Nimesahaulika miongoni mwao kama mtu aliyekufa,
nimekuwa kama chombo cha mfinyanzi kilichovunjika.
13Kwa maana nimesikia maneno niliyosingiziwa na wengi;
vitisho viko pande zote;
kwa kuwa wamefanya mashauri dhidi yangu,
na kula njama kuniua.
14Lakini mimi ninakutumaini wewe peke yako, Ee Mwenyezi Mungu;
nimesema, “Wewe ndiwe Mungu wangu.”
15Siku za maisha yangu ziko mikononi mwako,
uniokoe mikononi mwa adui zangu
na wale wanifuatiao.
16Mwangazie mtumishi wako uso wako,
uniokoe kwa ajili ya upendo wako usiokoma.
17Usiniache niaibike, Ee Mwenyezi Mungu,
kwa maana nimekulilia wewe,
bali waovu waaibishwe
na kunyamazishwa Kuzimu.
18Midomo yao isemayo uongo na inyamazishwe,
kwa maana kwa kiburi na dharau
wao husema kwa majivuno
dhidi ya wenye haki.
19Tazama jinsi wema wako ulivyo mkuu,
uliowawekea akiba wanaokucha,
unaowapa wale wanaokukimbilia
machoni pa watu wote.
20Unawahifadhi katika uvuli wa uwepo wako
kutokana na hila za wanadamu;
katika makao yako huwaweka salama
kutokana na ndimi za mashtaka.
21Atukuzwe Mwenyezi Mungu,
kwa kuwa amenionesha upendo wake wa ajabu
nilipokuwa katika mji uliozingirwa.
22Katika hofu yangu nilisema,
“Nimekatiliwa mbali na macho yako!”
Hata hivyo ulisikia kilio changu
ukanihurumia nilipokuita unisaidie.
23Mpendeni Mwenyezi Mungu ninyi watakatifu wake wote!
Mwenyezi Mungu huwahifadhi waaminifu,
lakini wenye kiburi huwalipiza kikamilifu.
24Kuweni hodari na mjipe moyo,
ninyi nyote mnaomtumaini Mwenyezi Mungu.
Iliyochaguliwa sasa
Zaburi 31: NENO
Kuonyesha
Shirikisha
Nakili
![None](/_next/image?url=https%3A%2F%2Fimageproxy.youversionapistaging.com%2F58%2Fhttps%3A%2F%2Fweb-assets.youversion.com%2Fapp-icons%2Fsw.png&w=128&q=75)
Je, ungependa vivutio vyako vihifadhiwe kwenye vifaa vyako vyote? Jisajili au ingia
Neno: Maandiko Matakatifu™ NMM™
Hakimiliki © 2018, 2024 na Biblica, Inc.
Imetumiwa kwa ruhusa.
Haki zote zimehifadhiwa duniani kote.
Kiswahili Contemporary Scriptures™
Copyright © 2018, 2024 by Biblica, Inc.
Used with permission. All rights reserved worldwide.