Chapa ya Youversion
Ikoni ya Utafutaji

Zaburi 89:19-37

Zaburi 89:19-37 NEN

Ulizungumza wakati fulani katika maono, kwa watu wako waaminifu, ukasema: “Nimeweka nguvu kwa shujaa, nimemwinua kijana miongoni mwa watu. Nimemwona Daudi, mtumishi wangu, na nimemtia mafuta yangu matakatifu. Kitanga changu kitamtegemeza, hakika mkono wangu utamtia nguvu. Hakuna adui atakayemtoza ushuru, hakuna mtu mwovu atakayemwonea. Nitawaponda adui zake mbele zake na kuwaangamiza watesi wake. Upendo wangu mkamilifu utakuwa pamoja naye, kwa Jina langu pembe yake itatukuzwa. Nitauweka mkono wake juu ya bahari, mkono wake wa kuume juu ya mito. Naye ataniita kwa sauti, ‘Wewe ni Baba yangu, Mungu wangu, Mwamba na Mwokozi wangu.’ Nitamteua pia awe mzaliwa wangu wa kwanza, aliyetukuka kuliko wafalme wote wa dunia. Nitadumisha upendo wangu kwake milele, na agano langu naye litakuwa imara. Nitaudumisha uzao wake milele, kiti chake cha enzi kama mbingu zinavyodumu. “Kama wanae wataacha amri yangu na wasifuate sheria zangu, kama wakihalifu maagizo yangu na kutoshika amri zangu, nitaadhibu dhambi yao kwa fimbo, uovu wao kwa kuwapiga, lakini sitauondoa upendo wangu kwake, wala sitausaliti uaminifu wangu kamwe. Mimi sitavunja agano langu wala sitabadili lile ambalo midomo yangu imelitamka. Mara moja na kwa milele, nimeapa kwa utakatifu wangu, nami sitamdanganya Daudi: kwamba uzao wake utaendelea milele, na kiti chake cha enzi kitadumu mbele zangu kama jua; kitaimarishwa milele kama mwezi, shahidi mwaminifu angani.”

Mipango ya Kusoma Bila Malipo na Ibada zinazohusiana na Zaburi 89:19-37